Faida za kuombea akili, ili kuimarisha Imani yako, maisha yako-2

May 12, 2022
Posted in Mafundisho
May 12, 2022 mwakasege

Faida za kuombea akili, ili kuimarisha Imani yako, maisha yako-2

Bwana Yesu asifiwe tena na tena…hata milele!
Leo, nataka nikuletee faida ya 2, inayotokana na mtu, kuombea akili zake. Hii ni sehemu ya mfululizo wa somo, tuliloanza kusoma tarehe 05/05/2022. Somo hilo lina kichwa kinachosema hivi: “Faida za kuombea akili, ili kuimarisha Imani yako, maisha yako”.
Faida ya 2 ya kuombea akili ni: “Kuziwezesha akili zako, zikubali kufanya kazi, chini ya uongozi wa amani ya Kristo”.
Biblia inasema katika Wafilipi 4:6, 7 ya kuwa: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu”.
“Akili zote” katika mstari huu ina maana fikra zote, na mawazo yote, na mitazamo yote, na uelewa wote, na ufahamu wote unaotokana na akili!
Hebu tuitizame kwa pamoja faida hii, kwa kuangalia mfano wa eneo lifuatalo:
“Kutafuta uongozi wa Mungu, juu ya jambo lolote”.
Mithali 23:4b inasema: “…acha kuzitegemea akili zako mwenyewe”. Na Mithali 3:5 inasema: “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe”.
Ingawa Biblia inaturuhusu, na kutuhimiza kuzitumia akili (Waebrania 5:14), lakini inatukataza tusizitegemee akili. Biblia inatuhimiza tuitumie “amani ya Mungu”, kuthibiti matumizi ya “akili zote” (Wafilipi 4:7).
Na kwa sababu hiyo, hutakiwi kuzitegemea akili (au fikra au mawazo), katika kutafuta uongozi wa Mungu, juu ya jambo lolote, bali tegemea amani ya Kristo, katika kuchagua ni fikra ipi ya kuifuata, au ni wazo lipi la kulifuata.
Hii ni kwa sababu, fikra na mawazo katika akili zako, si za kutegemewa kukuongoza, bila amani ya Mungu kuhusika!
Biblia inasema: Katika kila wazo, au fikra, au neno…“Utafute amani ukaifuate” (Zaburi 34:14). Na kwa sababu hiyo – “mtaongozwa na amani” (Isaya 55:12b).
Na ikiwa fikra, au wazo, vinakuongoza kwenye njia iliyopotoka, nje ya Mungu, utajikuta umekosa amani moyoni mwako!
Hii ni kwa sababu, wale wapitao katika njia iliyopotoka, hawana amani mioyoni mwao (Isaya 59:8). Tena “Wala njia ya amani hawakuijua” (Warumi 3:17).
Angalizo: Fikra yo yote moyoni mwako, isiyokubali kutawaliwa na kuongozwa na amani ya Kristo, usiifuate! Na usilifuate wazo lolote moyoni mwako, lisilokubali kutawaliwa, na kuongozwa na amani ya Kristo!
Kumbuka:
Jizoeze kuombea akili zako, na fikra zako, na mawazo yako, na mtazamo wako, vikubali kutawaliwa, na kufanya kazi chini ya amani ya Mungu, iliyo moyoni mwako kwa njia ya Yesu Kristo. Akili zako unapozitumia, zisipotoa ushirikiano kwa amani ya Mungu ndani yako, ni rahisi zikakupotosha na wakati huo huo usijue kama umepotoka!

TUNGEPENDA KUSIKIA KUTOKA KWAKO

Karibuuwasiliane nasi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu huduma ya MANA.