Welcome to our Blog

The daily Post

Read Our Blog

Faida ya 3 ya kuombea akili za mtu.

Leo tuangalie faida ya 3 ya kuombea akili za mtu. Faida hiyo ya 3 ni:
“Mungu azisaidie akili zako, ziwe na hali ambayo hatazikataa bali atazikubali”.
Mungu anasema hivi: “Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, na akili zao wenye akili nitazikataa” (1 Wakorintho 1:19).
Mungu anapozikataa “akili zao wenye akili”, ina maana hatashirikiana nazo katika utendaji wake! Mtu mwenye akili hizo, anaweza kuendelea kuzitumia akili hizo, lakini ya kwamba, atafanya akifanyacho, bila Mungu kuhusika na afanyacho, na bila Mungu kuwa upande wake, kwenye hicho afanyacho!
Zipo sababu kadhaa, zinazoweza kumfanya Mungu, azikatae “akili zao wenye akili”. Lakini kufuatana na mstari tuliosoma hapa juu, tunaona kuwa, aina ya hekima, inayotoka ndani ya akili, ina uhusiano mkubwa na Mungu kuzikataa akili.
Tukilitazama jambo hili kwa mtazamo huu, tutaona sababu kadhaa zifuatazo, zinazomfanya Mungu azikatae “akili zao wenye akili”!
Sababu ya 1:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu zinafanya kazi na hekima isiyo yake! Kufuatana na Ufunuo wa Yohana 17:9, akili zinatakiwa zifanye kazi na hekima ya Mungu. Hii ni kwa kuwa, akili ziliumbwa na Mungu (Ayubu 32:8), na kwa ajili hiyo, hekima inayotumika, ni lazima iwe ya Mungu.
Akili ikitumia hekima isiyo ya Mungu, Mungu anaiharibu hekima hiyo, na kuzikataa akili husika!
Sababu ya 2:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu akili zinatumia “hekima” ambayo imeuzarau msalaba wa Yesu na kuuona ni “upuuzi” (1 Wakorintho 1:22, 23).
Akili haifanyi sawa kushirikiana na hekima, inayodharau na kupuuzia msalaba wa Yesu, wakati biblia inasema msalaba huo ni “nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu” (1 Wakorintho 1:24).
Akili inapotumia hekima ya namna hii – kama ya Wayunani, Mungu anaiharibu hekima hiyo, na kuzikataa akili zao wenye akili, zilizobeba na kutumia hekima hiyo.
Sababu ya 3:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, kwa sababu hazimpi Yesu nafasi anayostahili, kama msingi wa maisha ya kila siku ya mtu, na msingi wa kazi za kila siku za mtu.
Biblia inatujulisha ya kuwa, Mungu aliiweka misingi ya nchi kwa kutumia hekima yake (Mithali 3:19). Na kwa ajili hiyo, akili za mtu zinatakiwa zimpe Yesu, nafasi ya kuwa msingi wa kila eneo la maisha ya mtu. Hii ni kwa kuwa, msalaba umemfanya Yesu awe “kwetu hekima itokayo kwa Mungu” (1 Wakorintho 1:30). Na kwa sababu hiyo, chochote ukifanyacho bila kutumia hekima ya Yesu, hakitakuwa na msingi imara.
Sababu ya 4:
Mungu anazikataa akili zao wenye akili, pale zisipotoa nafasi, kwa hekima ya Mungu itumike kumsaidia mtu: Kujua wakati wa kuongea; kujua namna ya kuongea; na kujua wakati wa kunyamaza kimya.
Biblia inasema: Mungu anawapa watu wake, “Kinywa na hekima” (Luka 21:14), ili wajue cha kusema, na wakati wa kusema, na namna ya kusema.
Lakini pia, biblia inatujulisha ya kuwa, kuna “kunyamaza” ambako ni matokeo, ya hekima ndani ya mtu, inayomsukuma anyamaze asiongee!
Imeandikwa hivi: “Laiti mngenyamaza kabisa! Hilo lingekuwa hekima kwenu” (Ayubu 13:5).
Kumbuka: Unapoombea Mungu azisaidie akili zako, ziwe na hali ambayo hatazikataa, bali atazikubali, usisahau kuomba toba kwake, ikiwa mojawapo ya sababu hizo nne, inakuhusu, au zote zinakuhusu.
Hii itampa Mungu nafasi ya kukusamehe, na kujibu maombi haya juu ya akili zako!

Faida za kuombea akili, ili kuimarisha Imani yako, maisha yako-2

Bwana Yesu asifiwe tena na tena…hata milele!
Leo, nataka nikuletee faida ya 2, inayotokana na mtu, kuombea akili zake. Hii ni sehemu ya mfululizo wa somo, tuliloanza kusoma tarehe 05/05/2022. Somo hilo lina kichwa kinachosema hivi: “Faida za kuombea akili, ili kuimarisha Imani yako, maisha yako”.
Faida ya 2 ya kuombea akili ni: “Kuziwezesha akili zako, zikubali kufanya kazi, chini ya uongozi wa amani ya Kristo”.
Biblia inasema katika Wafilipi 4:6, 7 ya kuwa: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu”.
“Akili zote” katika mstari huu ina maana fikra zote, na mawazo yote, na mitazamo yote, na uelewa wote, na ufahamu wote unaotokana na akili!
Hebu tuitizame kwa pamoja faida hii, kwa kuangalia mfano wa eneo lifuatalo:
“Kutafuta uongozi wa Mungu, juu ya jambo lolote”.
Mithali 23:4b inasema: “…acha kuzitegemea akili zako mwenyewe”. Na Mithali 3:5 inasema: “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe”.
Ingawa Biblia inaturuhusu, na kutuhimiza kuzitumia akili (Waebrania 5:14), lakini inatukataza tusizitegemee akili. Biblia inatuhimiza tuitumie “amani ya Mungu”, kuthibiti matumizi ya “akili zote” (Wafilipi 4:7).
Na kwa sababu hiyo, hutakiwi kuzitegemea akili (au fikra au mawazo), katika kutafuta uongozi wa Mungu, juu ya jambo lolote, bali tegemea amani ya Kristo, katika kuchagua ni fikra ipi ya kuifuata, au ni wazo lipi la kulifuata.
Hii ni kwa sababu, fikra na mawazo katika akili zako, si za kutegemewa kukuongoza, bila amani ya Mungu kuhusika!
Biblia inasema: Katika kila wazo, au fikra, au neno…“Utafute amani ukaifuate” (Zaburi 34:14). Na kwa sababu hiyo – “mtaongozwa na amani” (Isaya 55:12b).
Na ikiwa fikra, au wazo, vinakuongoza kwenye njia iliyopotoka, nje ya Mungu, utajikuta umekosa amani moyoni mwako!
Hii ni kwa sababu, wale wapitao katika njia iliyopotoka, hawana amani mioyoni mwao (Isaya 59:8). Tena “Wala njia ya amani hawakuijua” (Warumi 3:17).
Angalizo: Fikra yo yote moyoni mwako, isiyokubali kutawaliwa na kuongozwa na amani ya Kristo, usiifuate! Na usilifuate wazo lolote moyoni mwako, lisilokubali kutawaliwa, na kuongozwa na amani ya Kristo!
Kumbuka:
Jizoeze kuombea akili zako, na fikra zako, na mawazo yako, na mtazamo wako, vikubali kutawaliwa, na kufanya kazi chini ya amani ya Mungu, iliyo moyoni mwako kwa njia ya Yesu Kristo. Akili zako unapozitumia, zisipotoa ushirikiano kwa amani ya Mungu ndani yako, ni rahisi zikakupotosha na wakati huo huo usijue kama umepotoka!

Faida za kuombea akili, ili kuimarisha imani yako, na maisha yako-1

Bwana Yesu asifiwe
Tunaamini unaendelea vizuri. Leo nataka nianze kukuletea mfululizo wa masomo, yanayohusu: “Faida za kuombea akili, ili kuimarisha imani yako, na maisha yako”. Ninapoziandika faida hizi, siziandiki kwa mtiririko wa umuhimu. Naziandika kwa mtiririko wa mfuatano wa kiuandishi tu, faida zote ni muhimu!

Faida ya 1 ya kuombea akili:

MUNGU AKUSAIDIE, KUJUA MATUMIZI YA AKILI ALIZOKUPA, ILI UWEZE KUZITUMIA IPASAVYO, KAMA ALIVYOKUSUDIA.
Mungu alipomuumba mtu, alimuumba awe jumlisho la roho, na nafsi, na mwili (2 Wakorintho 7:1). Mtu ni roho, anayo nafsi, na anakaa ndani ya mwili!
Mtu aliumbwa aweze kuishi, kwenye ulimwengu mbili kwa wakati mmoja – yaani ulimwengu wa kiroho, na ulimwengu wa kimwili kwa pamoja, na kwa wakati mmoja.
Mtu aliumbwa awe roho, ili kwa njia ya roho, aweze kuishi katika ulimwengu wa roho (Mwanzo 1:26, 27). Na kwa mwili wake, aweze kuishi katika ulimwengu wa kimwili (Mwanzo 2:7).
Na mtu alipewa nafsi, ili iwe “kiungo”, kati ya roho na mwili. Na kwa ajili ya jukumu hilo, nafsi ni kiungo muhimu cha mtu, katika kuunganisha maisha yake ya kiroho, na ya kimwili.
Ndiyo maana roho ya mtu, ndiyo iliyoumbwa kwanza (Mwanzo 1:27). Mwili wa mtu, uliumbwa wa pili (Mwanzo 2:7a). Na nafsi ya iliumbwa ya tatu (Mwanzo 2:7b)
Biblia inasema: “Bwana Mungu…, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai” (Mwanzo 2:7). Na ukisoma Ayubu 32:8; utasoma maneno haya: “Lakini imo roho ndani ya mwanadamu, na pumzi za Mwenyezi huwapa akili”.
Mistari hiyo miwili, inatupa kujua, na kuamini kuwa, akili imo ndani ya Nafsi!
Lakini pia, ni vizuri ujue ya kuwa, akili siyo ubongo, na ubongo siyo akili; ingawa vyote viwili viliumbwa ili vifanye kazi kwa kushirikiana! Ubongo umo katika mwili, na akili imo katika nafsi!
Biblia inatuelekeza tusizitegemee akili! Imeandikwa katika Mithali 3:5, 6; kuwa: “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyoosha mapito yako”.
Na Mithali 23:4 inasema: “…acha kuzitegemea akili zako mwenyewe”.
Pamoja na maagizo ya biblia, kwamba tusizitegemee akili, inatuhimiza pia, kuwa tuzitumie akili! Hii inatujulisha kuwa, Mungu aliziumba akili ndani ya kila mtu, ili azitumie, lakini asizitegemee!
Biblia inasema: “…Kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya” (Waebrania 5:13, 14).
Faida mojawapo ya kuombea akili, ni ili Mungu akusaidie kujua matumizi ya akili alizokupa, ili uweze kuzitumia hizo akili, kama alivyokusudia!
Tena, kumbuka, bila msaada wa Mungu, si rahisi sana ukaweza kuzitumia akili bila kuzitegemea! Lakini Mungu, anao uwezo wa kukusaidia, uweze kuzitumia akili, na usizitegemee, bali umtegemee Yeye!
Ombea akili ili ujue matumizi yake! Kitu usichojua matumizi yake, ni rahisi kukitumia vibaya; au hutakitumia kwa kiwango kinachotakiwa! Na kitu ulichonacho, na huijui faida yake kwako, si rahisi pia kukikumbuka kukiombea ipasavyo! Zijue faida za akili, ili uweze kukumbuka kuziombea mara kwa mara!
Tuzidi kuombeana katika hili!

TUNGEPENDA KUSIKIA KUTOKA KWAKO

Karibuuwasiliane nasi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu huduma ya MANA.