SALAMU ZA PASAKA 2024

March 29, 2024
Posted in Mafundisho
March 29, 2024 mwakasege

SALAMU ZA PASAKA 2024

Bwana Yesu asifiwe!
Maneno ambayo Yesu aliyasema akiwa katika bustani ya Gethsemane masaa machache kabla Yuda hajamsaliti, yanatupa msukumo mkubwa wa kutaka kujifunza zaidi juu ya kuombea majaribu.

Yesu alisema hivi: “Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu” (Mathayo 26:41).

Leo nataka tujifunze umuhimu wa “Kumwomba Mungu akupe kujua chanzo cha jaribu linalokukabili, na akupe msaada wa kulishinda”.
Hili ni muhimu kulijua kwa sababu, kujua chanzo cha jaribu, kunakupa na kunakuwezesha, uwe na msingi mzuri wa namna ya kulishinda jaribu husika.

Ni muhimu sana kukijua chanzo cha jaribu linalokuhusu. Hii ni kwa sababu, ingawa yapo majaribu ya aina “mbalimbali” (Yakobo 1:2), lakini majaribu hayo yanalenga kukijaribu kitu kimoja nacho ni “Imani” (Yakobo 1:3) ya yule anayejaribiwa!

Ukisoma na ukitafakari juu ya vyanzo vya majaribu kibiblia, utaona ya kwamba, ukikijua chanzo cha jaribu, utajikuta unajifunza kulitazama na kuliombea jaribu husika, kutoka kwenye nia ya lengo la anayekujaribu, kukuletea jaribu linalolenga imani yako.
Hebu tujifunze zaidi kwa kuangalia vyanzo vifuatavyo vya majaribu:

Mfano wa 1:
Chanzo cha jaribu kinapokuwa ni shetani.
Tunasoma katika Mathayo 4:1 ya kwamba: “Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na ibilisi”. Maneno ya mstari huu, yanatupa kufahamu ya kuwa chanzo kimojawapo ni Ibilisi au Shetani.
Lengo kubwa la Shetani kuijaribu imani ya mtu aliyonayo ndani ya Yesu Kristo, ni ili imani hiyo ishindwe kumsaidia katika jaribu hilo, hatimaye apate sababu ya “kujitenga na imani” hiyo (1 Timotheo 4:1).

Lakini, hata kama hatajitenga na imani, basi imani aliyonayo katika Yesu Kristo, iendelee kupungua nguvu, na ikibidi imani itindike au iishe kabisa (Luka 22:31, 32).

Biblia inasema, “Imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo” (Warumi 10:17). Hii ina maana ya kuwa jaribu la shetani kwenye imani yako, linalenga kukufanya upoteze tumaini lako kwenye uwezo wa Mungu kutimiza ahadi zake.

Tukisoma habari za kujaribiwa kwa Yesu na shetani, katika Mathayo 4:1 – 11 na katika Luka 4:1 – 13, tunajifunza mambo yafuatayo juu ya kushughulika na majaribu ambayo chanzo chake ni shetani:

Jambo la 1: Yesu aliweka nia ya kumshinda shetani kama mjaribu, katika lengo alilokuwa nalo (shetani), la kutaka Yesu aache kumtegemea Mungu na neno lake.
Ndiyo maana katika majaribu yote matatu ya Shetani, Yesu alimjibu Shetani kwa kusema “imeandikwa” (Mathayo 4:4, 7), ili Shetani ajue ya kuwa hata katikati ya majaribu, ataendelea kumtegemea Mungu na kulitumainia neno lake
Na wewe fanya vivyo hivyo unapokuwa katika jaribu, kama vile Yesu alivyofanya. Tafakari na kukiri mistari ya neno la Mungu, inayoahidi Mungu kukupa ushindi katika jaribu hilo. Na Mungu ataliangalia neno lake hilo, na kukutimizia (Yeremia 1:12).

Jambo la 2: Shetani alimsemesha Yesu, kwa namna ambayo, alitaka amuone Mungu siyo mwaminifu. Lakini Yesu alikataa wazo hilo la shetani kwa njia ya neno la Mungu na kwa maombi.

Na wewe unapoona jaribu linakuletea mawazo ya kuona kuwa, kumtegemea Mungu na neno lake hakujakusaidia kushinda jaribu hilo, na kwa ajili hiyo unajikuta unapoteza nia ya kuendelea na jambo ulilokuwa unalifanya, ujue nyuma ya jaribu hilo kuna Shetani!

Na inawezekana kwako wewe, imani yako ikawa bado ina nguvu hata kama ni kidogo; lakini wakati huo huo imani za wanaokuzunguka, nguvu za imani zao zimeisha. Na watu kama hao, utakuta wanazungumza na wewe maneno yanayokutaka uache kumtegemea Mungu wako, kwa kuwa wanaona ameshindwa kukusaidia.

Unakumbuka alichosema mke wa Ayubu kwa Ayubu baada ya imani yake kuishiwa nguvu, walipokuwa wamesongwa na majaribu?

Biblia inasema mke wa Ayubu alimwambia mume wake hivi: “Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye (Ayubu) akamwambia, wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu wanenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake” (Ayubu 2:9, 10).

Hali hii iliwahi kumpata Daudi, kama tunavyosoma katika Zaburi 42:1 – 4. Je, kuna jaribu unalolipitia na unasikia kukata tamaa? Usikate tamaa na endelea kumwomba Mungu juu hali unayoipitia, naye atakusaidia (Luka 18:1).

Jambo la 3: Neno alilokuwa analitumia Yesu, alipokuwa anajaribiwa na Shetani, lililenga kuua nguvu za Shetani kwanza, ili kulifanya jaribu lipoteze nguvu za kumjaribu Yesu.

Na ndio maana kabla ya Yesu kumwambia Shetani kwa mara ya tatu kuwa “imeandikwa”; Yesu alimkemea kwanza Shetani ili aondoke.
Biblia inasema: “Ndipo Yesu alipomwambia, nenda zako shetani. Kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake, kisha Ibilisi akamwacha…” (Mathayo 4:10, 11).

Na tunaona pia ya kuwa Shetani alipokemewa na kuondoka, na majaribu pia yalikoma katika kipindi kile! Na wewe fanya vivyo hivyo! Ukijua ya kuwa ni shetani aliye chanzo cha jaribu lako, tumia neno la Mungu la biblia kumpinga, halafu mkemee na kumwamuru aondoke. Uwe na uhakika ataondoka!

Naamini umepata jambo la kukusaidia katika somo hili la leo.

Tunakutakia wiki njema ya sikukuu ya Pasaka.

 

TUNGEPENDA KUSIKIA KUTOKA KWAKO

Karibuuwasiliane nasi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu huduma ya MANA.