Pasaka ni jina la sadaka (Kutoka 12:11 na 1 Wakorintho 5:7). Pasaka ni chakula cha kiukombozi (Kutoka 12:11 na Yohana 6:35, 51, 55). Pasaka ni sikukuu yenye kukumbusha ukombozi wa Mungu kwa mwanadamu (Kutoka 12:11, 14 – 20 na Luka 22:19, 20).
Wakati wa pasaka, Mungu aliagiza kuwa, watu wanaokwenda kumwabudu, wasionekane mbele yake, “mikono mitupu” (Kutoka 23:15). Hii ikiwa na maana ya kuwa, wanatakiwa waonekane mbele zake, wakiwa na sadaka katika mikono yao!
Mungu akaahidi kuwafanyia mambo yafuatayo, wale watakaotoa sadaka wakati wa pasaka! Na ndiyo atakayokufanyia na wewe ukitoa sadaka kwa imani wakati wa pasaka:
Jambo-1
Mungu atakutumia Malaika wa kuwa pamoja nawe njiani, na kukulinda, na kukupigania dhidi ya adui zako, na dhidi ya watesi wako (Kutoka 23:20 – 23). Na kukusaidia upate urithi wa Mungu ulio haki yako.
Jambo-2
Mungu ataamsha kwa upya ndani yako, kiu ya kumtumikia Bwana Mungu (Kutoka 23:25).
Jambo-3
Mungu “atakibarikia chakula chako na maji yako” (Kutoka 23:25).
Jambo-4
Mungu atakuondolea “ugonjwa kati yako” (Kutoka 23:25).
Jambo-5
Mungu atakuponya na kukuepusha na matatizo ya uzazi na matatizo ya kizazi (Kutoka 23:26).
Jambo-6
Mungu atakufunika na utiisho wake, ambao atautumia kuwafadhaisha, na kuwafukuza mbele zako, adui zako, na wapinzani wako, wasikukwamishe kwenye kile ambacho anakusudia kukupa (Kutoka 23:27 – 29).
Jambo-7
Mungu atakusaidia upate maandalizi, ya kiroho, na ya kiakili, na ya kimwili, ili uweze kunufaika na vilivyopo katika “eneo”, ambalo amekuweka, au atakuweka kwa ajili yake (Kutoka 23:30).
Tafakari mambo haya saba
kwa namna ambayo imani itaongezeka ndani yako, ili unufaike na utoaji wako wa sadaka, wakati wa kipindi cha pasaka. Ni vizuri ujue pia, ya kuwa, mambo haya Mungu anaweza kukufanyia, kwa namna tofauti tofauti, wakati ambao si wa pasaka.
Tuzidi kuombeana. Tunakutakia pasaka njema!