SALAMU ZA PASAKA 2022

April 16, 2022
Posted in Mafundisho
April 16, 2022 mwakasege

SALAMU ZA PASAKA 2022

Bwana Yesu asifiwe milele!
Jambo mojawapo kubwa, na linalofanywa na wakristo walio wengi; wakati wa kipindi kama hiki cha ‘pasaka’, ni utoaji wa sadaka kwa Mungu.

Pasaka ni jina la sadaka (Kutoka 12:11 na 1 Wakorintho 5:7). Pasaka ni chakula cha kiukombozi (Kutoka 12:11 na Yohana 6:35, 51, 55). Pasaka ni sikukuu yenye kukumbusha ukombozi wa Mungu kwa mwanadamu (Kutoka 12:11, 14 – 20 na Luka 22:19, 20). 

Tukiyajua haya, inakuwa rahisi kuelewa, ni kwa nini ’Pasaka’ huwa inaambatana na utoaji wa sadaka, na ushiriki wa chakula cha Bwana; na sikukuu!
Ndani ya salamu hizi za pasaka za mwaka huu 2022, tunataka tukukumbushe juu ya mambo 7, ambayo Mungu, atawafanyia watoaji sadaka, wanaotoa sadaka wakati wa pasaka.

Wakati wa pasaka, Mungu aliagiza kuwa, watu wanaokwenda kumwabudu, wasionekane mbele yake, “mikono mitupu” (Kutoka 23:15). Hii ikiwa na maana ya kuwa, wanatakiwa waonekane mbele zake, wakiwa na sadaka katika mikono yao!
Mungu akaahidi kuwafanyia mambo yafuatayo, wale watakaotoa sadaka wakati wa pasaka! Na ndiyo atakayokufanyia na wewe ukitoa sadaka kwa imani wakati wa pasaka:

Jambo-1

Mungu atakutumia Malaika wa kuwa pamoja nawe njiani, na kukulinda, na kukupigania dhidi ya adui zako, na dhidi ya watesi wako (Kutoka 23:20 – 23). Na kukusaidia upate urithi wa Mungu ulio haki yako.

Jambo-2

Mungu ataamsha kwa upya ndani yako, kiu ya kumtumikia Bwana Mungu (Kutoka 23:25).

Jambo-3

Mungu “atakibarikia chakula chako na maji yako” (Kutoka 23:25).

Jambo-4

Mungu atakuondolea “ugonjwa kati yako” (Kutoka 23:25).

Jambo-5

Mungu atakuponya na kukuepusha na matatizo ya uzazi na matatizo ya kizazi (Kutoka 23:26).

Jambo-6

Mungu atakufunika na utiisho wake, ambao atautumia kuwafadhaisha, na kuwafukuza mbele zako, adui zako, na wapinzani wako, wasikukwamishe kwenye kile ambacho anakusudia kukupa (Kutoka 23:27 – 29).

Jambo-7

Mungu atakusaidia upate maandalizi, ya kiroho, na ya kiakili, na ya kimwili, ili uweze kunufaika na vilivyopo katika “eneo”, ambalo amekuweka, au atakuweka kwa ajili yake (Kutoka 23:30).

Tafakari mambo haya saba

kwa namna ambayo imani itaongezeka ndani yako, ili unufaike na utoaji wako wa sadaka, wakati wa kipindi cha pasaka. Ni vizuri ujue pia, ya kuwa, mambo haya Mungu anaweza kukufanyia, kwa namna tofauti tofauti, wakati ambao si wa pasaka.

 

Ukiwa msomaji wa biblia, utakuwa unajua ya kuwa, katika sikukuu kadhaa alizoziamuru Mungu, zifanywe na wanadamu, kuna ahadi alizoziahidi kuzitoa “kwa pamoja” (Collectively)-kwa washiriki wa sikukuu hizo. Na sikukuu mojawapo, ni hii ya Pasaka!

Tuzidi kuombeana. Tunakutakia pasaka njema!

 

TUNGEPENDA KUSIKIA KUTOKA KWAKO

Karibuuwasiliane nasi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu huduma ya MANA.